Mwenyekiti wa Makampuni ya Vigor ya Zanzibar ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Mpendae Mhe. Toufiq Salim Turky amekutana na Waziri wa Utalii na Mazingira wa Comoro Mhe. Abubakar ben Mahamoud na kumueleza azma yake ya kuongeza uwekezaji katika sekta ya hoteli nchini humo.
Mheshimiwa Turky ambaye tayari amewekeza Comoro katika sekta za Nishati na mifumo ya Fedha na awali alikuwa mwendeshaji wa hoteli kubwa zaidi nchini hapa yuko nchini Comoro kwa ziara ya kibiashara ambapo ameeleza azma yake ya kuongeza wigo wa uwekezaji wa makampuni yake ili wawe na hoteli kadhaa za hadhi ya juu nchini hapa.Mazungumzo yake na Waziri wa Utalii yalihudhuriwa pia na Balozi wa Tanzania nchini Comoro Mhe. Saidi Yakubu na Shaaban Battash, Mjumbe wa Baraza la Ulamaa, Zanzibar.
Kwa upande wake, Mheshimiwa Waziri Mahamoud alimhakikishia Mheshimiwa Turky kuwa Comoro kwa sasa ina uhitaji mkubwa wa wawekezaji katika sekta hiyo na amefika wakati muafaka ambapo nchi hiyo inajiandaa kuwa mwenyeji wa mashindano ya michezo ya Baharini mwaka 2027 na hoteli nyingi na huduma nyinginezo vitahitajika.